UUNDAJI WA MANENO


Uundaji wa maneno ni mabadiliko ya istilahi na muundo unaosababishwa na mabadiliko ya sayansi na tekinolojia katika Nyanja mbalimbali za jamii ili kukidhi dhima ya lugha kama chombo kinachojitosheleza katika mawasiliano. Ili kukidhi haja hii kuna mbinu mbalimbali zinazotumika katika uundaji na ukuzaji wa istilahi ya maneno katika lugha. (Matinde 2012:110).

Hivyo basi uundaji wa maneno ni ujenzi au uzalishaji au utengenezaji wa maneno mapya. Uundaji wa maneno mapya husaidia kuongeza msamiati katika lugha ili kukidhi mahitaji ya mawasiliano. Uundaji wa maneno mapya husababishwa na mabadiliko ya kiuchumi, kisiasa, kiutamaduni na maendeleo ya kisayansi yanayotokea katika jamii. Kwa mfano tunayo maneno mapya kama vile ufisadi, uwekezaji, ujasiriamali, ukeketaji na mengine mengi kutokana na mabadiliko ya kijamii.
Zifuatazo ni mojawapo ya njia za uundajia wa maneno katika lugha ya Kiswahili:-

              I.             UTOHOZI:
Ni mbinu ambayo maneno kutoka lugha chanzi hutoholewa toka lugha chanzi na hatimaye hufanyiwa marekebisho kwa kufuata kaida au sheria za kifonolojia na kimofolojia za lugha pokezi kabla ya kutumiwa. Neno linapotoholewa hutamkwa na kuandikwa kwa utaratibu wa lugha pokezi,  hata hivyo maana ya neno lililotoholewa hubakia ileile ya awali. Matinde, (2012 :114).
Mifano:
KIINGEREZA
KISWAHILI
Switch
Swichi
Lorry
Lori
Budget
Bajeti
Agenda
Ajenda
Biology
Baolojia
Dollar
Dola
Oxygen
Oksijeni

 Ubora wa mbinu hii:
i)                    Mbinu hii ya utohozi ni mbinu rahisi ya kutumiwa katika uundaji wa msamiati. Mzungumzaji          yeyote anaweza kutumia mbinu hii hata bila kuhudhuria kozi yoyote ya isimu au kufundishwa.
ii)                  Maneno mengi huweza kuundwa kwa kutumia mbinu hii ili kukidhi mahitaji ya matumizi katika      lugha mbalimbali.

Udhaifu wa mbinu hii.
i)                    Mbinu hii hulemaza ubunifu wa wanajamii katika kuunda msamiati mpya wenye kuakisi    utamaduni wa jamii husika.
ii)                  Lugha tohoaji huonekana kukosa uasilia yaani lugha huonekana kuwa chotara.
iii)                Baadhi ya maneno katika Kiswahili ambayo yametoholewa kutoka lugha ya kiingereza katika lugha            ya Kiswahili hutamkwa kwa namna tofauti kabisa.
Mifano;
KIINGEREZA
KISWAHILI
Data
Data, deta
Dance
Densi, dansi
Bank
Bank, benki
Radio
Redio, radio

Hivyo basi, kutohoa maneno toka lugha nyingine ni ile hali ya lugha fulani kuchukua maneno toka lugha nyingine yaani kila lugha ina tabia ya kuchukua maneno toka lugha nyingine ili kukidhi mahitaji ya msamiati.

Maneno kutoka lugha nyingine yanapotoholewa hubadilishwa kimatamshi ili yafuate kanuni za lugha husika.
Katika lugha ya Kiswahili maneno yanayotoholewa hayana budi kusanifishwa na baraza la Kiswahili la Taifa ndipo yaruhusiwe kutumiwa rasmi.
Mifano mingine ya maneno yaliyotoholewa kutoka lugha nyingine ni kama ifuatayo:-
Dukani                        kihindi
Salamu                        kiarabu
Kitivo                          (kipare)
Ikulu                            (kigogo/kisukuma).
Bunge                          (kigogo).

        II.             TAFSIRI.
Matinde, (2012) anadai tafsiri ni mbinu ya kuunda maneno ambapo maneno au vifungu katika lugha chanzi hufasiriwa katika lugha lengwa. Ufasiri huu huzingatia muundo wa lugha pokezi.
Mifano,
KIINGEREZA
KISWAHILI
Free market
Soko huria
Ruling part
Chama tawala

Ubora wa mbinu hii.
Mbinu hii huzingatia kigezo cha maana zaidi kuliko muundo wa maneno yaliyochukuliwa toka lugha chanzi na kutafsiriwa huafiki utamaduni wa lugha lengwa. Hali hii husaidia katika kuunda maneno yenye maana iliyo wazi na inayokubalika katika lugha lengwa.

Udhaifu wa mbinu hii.
Mara nyingi huwa vigumu kutafsiri baadhi ya manenotoka lugha chanzi kwa kufuata kigezo maana.
Kuna uwezekano wa kupata tafsiri ambazo hazina maana wala mantiki katika lugha lengwa.
Mfano.
Kitchen party  -    sherehe ya jikoni.
Things fall apart  -   vitu vilivyoanguka na kutapakaa.

      III.            UFUPISHAJI:
Rubanza (1996) anaeleza kuwa baadhi ya majina ya maneno katika lugha nyingine za dunia hutokana na ufupishaji wa maneno yanavyotumiwa kwa pamoja kwa kutumia herufi au silabi za mwanzo tu za maneno hayo. Njia hii ameita Akronimu.
Matinde (2012) anaeleza kuwa ufupishaji ni mbinu ambayo hutokana na kitenzi ‘fupisha’ chenye maana ya kufanya kitu kiwe kifupi au kupunguza urefu wa kitu.
Kwa mujibu wa Rubanza (1996) njia ya ufupishaji imegawanyika katika sehemu kuu mbili kama ifuatavyo:-

      a.      Akronomi.
Kwa mfano katika Kiswahili tuna maneno ambayo yametokana na herufi au silabi za mwanzo za maneno kama vile:-
UKIMWI        -           Ukosefu wa Kinga Mwilini.
TUKI              -           Taasisi ya Uchunguzi wa Kiswahili.
BAKITA         -           Baraza la Kiswahili Tanzania.
TAKUKURU -           Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa.
KKKT             -           Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania.

            b.      Uhurutishaji.
Uhurutishaji ni tendo jingine linalokaribiana na tendo la akronimi, katika tendo hili vijisehemu vya maneno huwekwa pamoja kuunda neno jipya. Mfano katika lugha ya Kiswahili tunaweza kupata maneno kama vile:-
Chakula cha jioni    -               Chajio.
Hati za kukataza      -              Hataza.
Mama mdogo           -              Mamdo.
Chakula cha mchana -             Chamcha.
Vijisehemu vilivyowekwa pamoja si lazima viwe vyanzo vya maneno.

            c.       Ufupishaji Mkato (clipping).
Matinde, (2012) anatofautiana na Rubanza (1996) kwa kuongeza mbinu nyingine ya ufupishaji ambayo ni ufupisho mkato (clipping). Katika mbinu hii baadhi ya vipashio au silabi hudondoshwa na kuacha sehemu tu ya neno asilia.
Mifano.
NENO ASILIA
KIFUPISHO
Dar es salaam
Dar
Shemeji
Shem
Morogoro
Moro
Dada
Da
Binamu
Bina


       IV.            KUINGIZA MANENO YA LAHAJA NA LUGHA ZA KIBANTU.
Hiki ni chanzo kingine cha upatikanaji wa istilahi za Kiswahili.

Dhana ya Lahaja.
Lahaja ni namna tofautitofauti  za kuzungumza lugha moja. Aina hizi tofauti za kuzungumza lugha moja haziwazuii wazungumzaji kuelewana. Mgulu, (1999:17).

      a.        Kuingiza maneno kutoka lahaja za Kiswahili.
Mifano.
Wawe             -           kipate au kiamu
Mbolezi           -           kimvita.
Tungomsele     -           kiamu

      b.      Kuchukua kutoka lugha nyingine za kibantu.
Njia ya kuchukua istilahi kutoka lugha ya kibantu imekuwa ikitumika kuongeza istilahi za Kiswahili.
Mifano.
Ngeli   -           Kihaya
Bunge -           kigogo
Ikulu    -           kisukuma

      V.            KUBUNI.
Matinde (2012) anasema ubunifu ni mbinu ya kubuni msamiati katika lugha husika na kurejelea dhana au vitu vipya ambavyo hapo awali havikuwepo katika jamii husika. Ni mbinu ambayo hutumiwa badala ya kuchukua maneno kutoka lugha nyingine. Mfano kubuni kwa kuongozwa na vigezo maalum kama ifuatavyo:-

Uakisi wa umbo la kirejelewa.
Kuna leksia za Kiswahili ambazo huakisi umbo la kiashiriwa.
Mifano ya maneno.
Neno ̔ Nyoka’ huibua taswira ya kitu kilichonyooka.
Neno ‘pembe kali’ hurejerea umbo lenye pembe iliyo na digrii pungufu ya 90.
Neno ‘kidole tumbo’ (appendix) huakisi umbo la sehemu ya mwili inayorejelewa ambayo ni kifuko  kama kidole ambacho kipo sehemu ya chini ya utumbo mkubwa.

Uakisi wa sauti au mlio.
Uakisi huu hubainika pale ambapo leksia huhusika kudhihirisha mfanano wa kisauti au mlio baina yake na kirejerewa.
Mifano.
Pikipiki            mlio, pik… pik… pik…
Kuku               mlio, ku… ku… ku…ku…
Cherehani        mlio, cherr…cherr…cherr…cherrr…

Uakisi wa tabia.
Baadhi ya leksia katika lugha huakisi tabia za kirejelewa, kwa mfano neno ‘Kifaurongo’ ambalo limeundwa kutokana na maneno mawili ‘kufa’ na ‘urongo’. Huyu ni mdudu apatiakanaye kwenye kokwa la embe ambaye akiguswa hujikunja na kukaa kimya kama amekufa. Hivyo basi neno kifaurongo huakisi tabia ya mdudu huyo.
Mfano mwingine ni ‘kinukamito’ ambayo imeundwa na maneno mawili ‘nuka’ na ‘mto’ hurejelea mtu anayeoa na kuacha  mara kwa mara (asiye na msimamo).

Uundaji wa Maneno
Katika sehemu zilizotangulia, tumeangalia kwa ujumla dhaha za msingi na kanuni zinazotumika katika taaluma ya mofolojia, na kutoa mifano kutoka lugha mbali mbali. Katika sehemu hii tutaangalia jinsi lugha zinavyotumia kanuni za namna hiyo katika kuunda maneno. Kwa kuanza mjadala, tuangalie maneno ya orodha mbili zifuatazo:



A
a) mtu
b) mti
c) kisu
d) ndizi
e) sema
f) imba
g) ona
B
a) somo
b) ushindi
c) kiongozi
d) mwanafunzi
e) semesha
f) imbia
g) onana
Maneno ya kundi (A) tunaweza kuyaita maneno-asili, kwa sababu hayakutokana na mashina au mizizi ya maneno mengine, yaani hakuna kipashio kilichoongezewa katika mzizi ili kuunda neno jipya. Lakini maneno ya kundi (B), tutakubaliana, yameongezewa vipashio vya ziada na vipashio hivyo vimesababisha kutokea kwa maneno mapya. Maneno ya kundi (B) tuyaite maneno-unde, kuyatofautisha na yale ya kundi (A). Ni muhimu kuona tofauti iliyopo kati ya maneno ya makundi haya mawili. Maneno yote ya hapo juu tunaweza kuyakatakata katika mizizi na viambishi, na kupata mofimu tofauti kwa kila neno. Jambo muhimu hapa ni kazi za vipashio vinavyounda maneno ya kundi (A) na vile vinavyounda maneno ya kundi (B). Baadhi ya wana-sarufi wanaweka tofauti kati ya uchambuzi wa maneno ya makundi haya kwa kuuita ule wa maneno ya kundi (A) MOFOLOJIA-AMBISHI, na ule wa kundi (B) MOFOLOJIA-UNDAJI. Tunaweza kusema kuwa kilichofanyika katika maneno ya kundi (A) ni kuweka viambishi katika mizizi ya manenu hayo, ili kuonyesha ngeli katika (a-d), na kuweka irabu /a/ kuonyesha udhihirisho wa kitenzi katika (e-g).
Maneno ya kundi (B) ni changamano zaidi. Maneno haya yamewekewa “viundaji”, yaani vipashio ambavyo kazi yake ni kuunda maneno mengine kutokana na mizizi hiyo hiyo. Hivyo neno {somo} ni nomino-unde, kwa sababu limetokana na kitenzi {soma}, na kipashio /-o-/ kilichowekwa baada ya mzizi {sem-} ni mofimu-undaji, na kikazi ni kiundaji-nomino. Neno “jipya” {somo} linaingia katika ngeli ya 5 na wingi wake ni {masomo} ambalo linaingia katika ngeli ya 6. Katika (B) neno {ushindi} linatokana na mzizi {shind-} ambao umeongezewa kiundaji nomino /-i-/ na kuwekewa kiambishi ngeli /u-/, na hivyo kuliingiza neno hilo katika ngeli ya “nomino dhahinia” iliyo na maneno mengine kama {uuri, ukubwa} n.k. Neno la (c) {kiongozi} tumekwisha lijadili katika 4.0 hapo juu, nalo linatokana na mzizi wa kitenzi {ongoz-} ambao umewekewa kiundaji-nomino /-i/ kama neno lililotangulia, lakini limepewa kiambishi ngeli /ki-/. Neno linalofuata, {mwanafunzi} ni changamano zaidi kwa sababu linatokana na mizizi ya maneno mawili {-ana} na {funz-}. Mzizi wa neno la kwanza ndio umechukua kiambishi-ngeli /mu-/, ambapo lile la pili ndilo linachukua kiundaji /-i/. Maneno kama haya yanaitwa ambatano, kwa vile kimsingi ni maneno mawili yaliyowekwa pamoja ({mwana} na {mfunzi}).
Mifano hii michache inaonyesha njia tofauti zinazotumiwa kuunda nomino za Kiswahili kutokana na maneno ya makundi mengine. Kanuni za uundaji wa maneno ni tofauti katika kila lugha, lakini uundaji wa maneno ni jambo la kawaida sana. Kwa mfano, maneno yafuatayo ya Kiingereza ni maneno-unde: {childhood, cleanllness, helpful} n.k. (Kutokana na maneno {child, clean, help}). Kwa wana-sarufi wengi, mofolojia-undaji hasa inashughulikia kanuni za namna hii katika lugha tofauti, yaani kanuni za uundaji wa maneno ya kundi moja kutokana na mizizi ya makundi mengine tofauti.
Uingizaji wa maneno (22.B:e-g) hapo juu katika mofblojia-undaji unaleta utata kwa sababu maneno haya yanabaki katika kundi la vitenzi na hivyo si “tofauti” na vitenzi-sahili kama {sema, imba, ona} (lakini angalia mjadala katika 4.4). Hata hivyo, kinadharia, hakuna tofauti kati ya kanuni za uundaji zinazotumika katika maneno haya na zile zinazotumika katika maneno ya (B: a-d). Kama vile ambavyo tumeweza kuainisha viundaji nomino -/i/ na /-o/, tunaweza kuainisha viundaji-vitenzi /-esh-/, /-i-/, na /-an-/ ambavyo vimeongezwa katika mizizi ya vitenzi-sahili {sem-a, imb-a, on-a}. Viundaji hivi pia vinatumika katika kuunda vitenzi vya Kiswahili kutoka makundi mengine ya maneno, kama sifa na nomino: {safi: safisha; fupi: fupisha; neema: neemesha}, n.k. Katika msingi huo basi, {sema} na {semesha} ni maneno mawili tofauti kama yalivyo {ongoza} na {kiongozi}. Hivyo tunaweza kusema kuwa neno {semesha} ni kitenzi-unde kinachotokana na mzizi {sem-} ambao umeongezewa kiundaji {-esh-}; na maneno mengine tunaweza kuyaelezea kwa njia kama hiyo.
Maneno-unde katika lugha kama ya Kiswahili ni mengi sana, na jambo hili ni muhimu kwa sababu linasaidia kurahisisha mawasiliano. Mzungumzaji anaweza kuhusisha mara moja maana ya neno-unde kutokana na maana anayoijua ya neno-sahili lililokuwa msingi. Vile vile, viundaji katika lugha, kila vinapotokea, vinabakia na maana karibu ile ile, hivyo hata kama mzungumzaji hajalisikia neno-unde kabla, anaweza kubuni maana yake ikiwa anajua maana ya shina la msingi. Kwa mfano, si vigumu kwa mjua-Kiswahili kuona mshikamano uliopo kati ya maneno yafuatayo: {imba: imbia: imbisha: imbika: wimbo: mwimbaji: uimbaji}, kwa sababu anajua maana ya shina {imba} na anajua “maana” ya viundaji vilivyotumika.
Katika utangulizi tulisema kuwa mojawapo ya maswali ambayo taaluma ya mofolojia inapaswa kuyajibu ni uhusiano uliopo kati ya maana ya neno-changamano na maana za vipashio vinavyolijenga. Katika kuangalia neno moja moja, tunasisitiza zaidi taarifa za kisarufi zinazobebwa na vipashio vinavyolijenga neno hilo. Kwa mfano, neno {masomo} limejengwa na mofimu tatu: /ma-/ ambayo ni kiambishi ngeli, ngeli ya sita; /som-/ mzizi; na /-o/ kiundaji-nomino. Vipashio hivi ndivyo vinavyolipa neno hili maana maalumu na hivyo kulitofautisha na maneno mengine yanayochangia visehemu vinavyoliunda kama : {somo} (umoja wa {masomo}); {maneno} (linachangia /ma-/ na /o/); {somea} (linachangia mzizi /som/) n.k.
Kuna swali lingine ambalo tulisema wana-sarufi wanapaswa kulishughulikiakatika taaluma ya mofolojia, nalo ni uhusiano uliopo kati ya maneno ya lugha moja. Ni dhahiri kuwa kuna uhusiano wa ndani kati ya maneno hayo ambao unatawaliwa na kanuni maalumu. Uhusiano wa aina ya kwanza ni ule wa kundi. Kwa mfano, tukisema kuwa neno mtu ni nomino, ni kwamba tumekwishaliingiza katika kundi la NOMINO, na hivyo kukiri kuwa linaingia katika uhusiano maalumu na maneno mengine ya kundi hilo, yaani linashiriki katika sifa zile zinazotofautisha maneno ya kundi hilo na maneno ya makundi mengine katika lugha hiyo moja. Huu ni uhusiano wa msingi katika lugha zote, kwa sababu kushiriki kwa neno fulani katika kundi kunatawala matumizi ya neno hilo katika sarufi nzima ya lugha.
Uhusiano wa aina nyingine ni kama tuliouona katika sehemu hii, kwa mfano, uhusiano kati ya maneno-sahili na maneno-unde yanayochangia mzizi mmoja. Mpaka sasa, mahusiano haya tumeyaangalia kwa ujumla tu, lakini itakuwa imedhihirika kuwa kuna kanuni nyingi tofauti ambazo zinatumika katika uundaji wa maneno na ni muhimu kuweza kuzielezea kwa uwazi ili kuona jinsi zinavyohusiana na kanuni zinazotawala katika lugha nyingine. Kwa kufanya hivyo, huenda tukaweza kuunda kanuni za mofolojia ya lugha-jumla. Tutazijadili kanuni hizo katika sehemu inayofuata.


SARUFI: Matumizi ya Lugha
HITIMISHO:
Kwa ujumla uundaji wa maneno hupanua mipaka yake ya matumizi kwa kuongeza msamiati. Lugha nyingi ikiwemo lugha ya Kiswahili hutohoa baadhi ya msamiati kutoka lugha nyingine za dunia kutokana na mwingiliano wa watu. Lakini hata bila kutohoa maneno kutoka lugha nyinginezo kila lugha ikiwa pamoja na lugha ya Kiswahili kuna njia mbalimbali zzitumikazo katika kukuza msamiati wake.
MAREJELEO.
Masebo, J. A. (2010). Nadhari ya Lugha Kiswahili 1.Dar-Es Salaam: Nyambari Nyangwine
Publisher.
Matinde, R. S. (2012). Dafina ya Lugha Isimu na Natharia. Kwa Sekondari, Vyuo Vya Kati na
Vyuo Vikuu. Mwanza: Serengeti Educational Publishers.
Mgullu, R.S. (1999). Mtalaa wa Isimu, Fonetiko, Fonolojia na Mofolojia ya Kiswahili. Nairobi
Kenya: Longhorn Publishers.
Rubanza,Y. I.(1996). Mofolojia ya Kiswahili. Dar-Es Salaam: Chuo Kikuu Huria Cha Tanzania.



Maoni 17 :

  1. Matumizi 5 ya kiambajengo

    JibuFuta
  2. Nimefarijika sana na utajiri huu wa lugha nzuri na adhimu ya Kiswahili

    JibuFuta
    Majibu
    1. Naioenda mada hii kiukweli jmn

      Futa
  3. Nimefarijika sana maana nimepata nilichokuwa nakihitaji

    JibuFuta
  4. Asante sana kwa uchambuzi na ufafanuzi aula, kongole.

    JibuFuta
  5. Mifano ya misimu katika uundaji wa maneno ni nini
    Naombeni msaada sasa hivi

    JibuFuta
  6. Nimefarijika sana. Asanteni

    JibuFuta
  7. Kazi kuntu ✌️✌️

    JibuFuta
  8. Nashukuru sana

    JibuFuta
  9. Matatizo yepi yanapatikana katika uundaji wa maneno?

    JibuFuta
  10. eleza sababu za uundaji wa isitilahinza lugha ya kiswahili?

    JibuFuta
  11. Bora sana👍

    JibuFuta
  12. Munawarmuhdhar808@gmail.com17 Januari 2024, 09:28

    Nzuri sana

    JibuFuta
  13. Munawarmuhdhar808@gmail.com17 Januari 2024, 09:28

    Nzuri sana

    JibuFuta